Usajili wa mbio za Rock City wazinduliwa Mwanza

By Gadiola Emanuel - 7:56:00 AM

Meya wa Jiji la Mwanza, Stanslaus Mabula akionyesha fomu ya kujisajili kushiriki mbio za kilomita tano zitakazofanyika Oktoba 26 baada ya kuzindua usajili wa washiriki wa mashindano ya Rock City Marathon jijini Mwanza, jana
 Meya wa Jiji la Mwanza, Stanslaus Mabula akiongea muda mfupi kabla ya kuzindua usajili wa washiriki wa mashindano ya Rock City Marathon jijini Mwanza jana ambapo alichukua fomu ya kujisajili kushiriki mbio za kilomita tano zitakazofanyika Oktoba 26.
 Mratibu wa mashindano ya mbio za Rock City Marathon 2014, Mathew Kasonta, akiongea wakati wa uzinduzi wa usajili wa washiriki wa mashindano hayo jijini Mwanza jana ambapo Mstahiki Meya wa Jiji la Mwanza, Stanslaus Mabula, alichukua fomu ya kujisajili kushiriki mbio za kilomita tano zitakazofanyika Oktoba 26.
 Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Riadha mkoa wa Mwanza, Charles Kimune, akiongea machache kabla ya kumkaribisha Mstahiki Meya wa jiji la Mwanza, Stanslaus Mabula, kuzindua usajili wa washiriki wa mashindano hayo jijini Mwanza jana ambapo Mabula alichukua fomu ya kujisajili kushiriki mbio za kilomita tano zitakazofanyika Oktoba 26.
Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Riadha mkoa wa Mwanza, Charles Kimune, akiongea machache kabla ya kumkaribisha Mstahiki Meya wa jiji la Mwanza, Stanslaus Mabula, kuzindua usajili wa washiriki wa mashindano hayo jijini Mwanza jana ambapo Mabula alichukua fomu ya kujisajili kushiriki mbio za kilomita tano zitakazofanyika Oktoba 26.

Meya wa Jiji la Mwanza, Stanslaus Mabula amekuwa mtu wa kwanza kujisajili Kanda ya Ziwa kushiriki mbio za Rock City Marathon, huku akiwataka viongozi kuhakikisha wanafufua mchezo huo ili kuurejesha kwenye hadhi yake kimataifa.


Akizindua usajili wa ushiriki wa mbio hizo jijini hapa jana, Mabula alisema mbio hizo zinalenga kutambua na kukuza vipaji vya riadha nchini, kutangaza vyanzo vya utalii na kuongeza kipato kwa vijana ikizingatiwa kuwa michezo ni mojawapo wa fursa za ajira.


“Mnajua jinsi tunavyohangaika kutangaza utalii wetu, lakini kupitia mashindano haya ambayo yapo kwenye kalenda ya mwaka ya Chama cha Riadha Tanzania (RT) tutatangaza utalii wetu kupitia mchezo huu,” alisema Mabula na kuongeza:


“Viwango vya riadha kwa miaka mitano tangu mashindano haya yaanzishwe vimekuwa vikipanda, ambayo pia ni faida kwa wadhamini ambao wanawekeza rasilimali watu na fedha, hivyo yamekuwa na mafanikio.”


Alisema angependa mshindi wa kwanza hadi watatu atoke jijini Mwanza ili kuendelea kutoa sifa kwa mkoa huu, lakini kubwa ni fursa ya vijana kujipatia kipato kwa sababu hivi sasa michezo ni biashara.


Mabula aliwapongeza wadhamini wa Rock City Marathon kwa mwaka huu kwa kusaidia kufanikisha uandaaji wa mashindano hayo kwa mara nyingine tena katika jiji la Mwana, akiwataja kuwa ni Shirika la Hifadhi ya Jamii (NSSF), Makampuni ya TSN kupitia kinywaji chake cha Chilly Willy pamoja na African Barrick Gold, IPTL, Air Tanzania, New Mwanza Hotel, Nyanza Bottling, Sahara Media Group, Continental decoders, New Africa Hotel, PPF, Tanapa na Tanzania Tourist Board. 
  

Waandaji wa mashindano hayo yanayotarajiwa kufanyika Oktoba 26, Kampuni ya Capital Plus International Ltd (CPI) wamegawa washiriki kwa madaraja mbalimbali; Mashindano kwa wote itakuwa kilomita 21, kilomita tano ni kwa ajili ya walemavu wa ngozi (Albino) pamoja na washiriki kutoka makampuni na mashirika mbali mbali, Wazee kuanzia umri wa miaka 55 watakimbia kilomita tatu na watoto chini ya umri wa 12 kilomita mbili.


Naye Kaimu Meneja wa Shirika la Hifadhi ya Jamii (NSSF) Mkoa wa Mwanza, Shaaban Luanda ambao ni wadhamini wakuu wa mashindano hayo alisema Kazi yao kuu ni kuhifadhi jamii, hivyo kupitia michezo wanaamini watakuwa wamelinda afya ya jamii.


Awali, akimkaribisha Mabula, Makamu Mwenyekiti wa chama cha riadha mkoa wa Mwanza, Charles Kimune alisema licha ya changamoto zinazokabili mashindano hayo kwa miaka mitano iliyopita, yamendelea kupata mafanikio.


Mratibu wa mbio hizo, Mathew Kasonta alisema, “Wote mnakaribishwa kuchukua fomu zinazopatikana katika ofisi za Capital Plus International zilizopo posta mpya jengo la ATC ghorofa ya tatu, Chuo cha Mtakatifu Agustino Mwanza, Ofisi zote za Utamaduni na Michezo wilaya ya Mwanza, Uwanja wa Nyamagana na pia zinapatikana kwenye tovuti ya www.therockcitymarathon.blogspot.com

  • Share:

You Might Also Like

0 comments